Image

   Mambo Muhimu ya kuzingatia wakati wa ujazaji fomu

  1. Mwombaji anatakiwa kuwa na anuani ya barua pepe ambayo ataitumia kujisajili na kupokea kiunga kitakachomuwezesha kukamilisha usajili wake.
  2. Mwombaji anatakiwa kuwa na nyaraka zisizopungua mbili zitakazotumika kuthibitisha utambulisho wake. Mfano wa nyaraka hizo ni; Cheti cha kuzaliwa n.k.
  3. Mwombaji anatakiwa kufanya “scanning” ya nyaraka zake na kuziweka katika muundo wa PDF (usiozidi kurasa moja kwa kila kiambatisho) au picha katika muundo wa JPG au PNG.
  4. Ni muhimu Mwombaji kujaza Namba yake ya simu ya mkononi.
  5. Mwombaji anatakiwa kuambatisha cheti cha kuzaliwa endapo amezaliwa Mwaka 1980 na kuendelea. Aidha, endapo Mwombaji amezaliwa kabla ya mwaka 1980 anatakiwa kuambatisha cheti cha kuzaliwa au “Affidavit”.
  6. Kwa Waombaji wenye majina mengine; ni vyema kuandika majina hayo ili endapo ikatokea uhitaji wa kurekebisha majina yake iwe rahisi kutambulika.
  7. Mwombaji anatakiwa kufahamu majina ya Baba na Mama yake mzazi.
  8. Mwombaji ambaye ana Namba za Utambulisho (NIN) za wazazi wake; anatakiwa kuweka viambata halisi (kwa wazazi waliokwishapata vitambulisho vya Taifa).
  9. Mwombaji anatakiwa kujua namba ya Nyumba, Mtaa na kata anayoishi.
  10. Kwa Watanzania walioko nje ya Nchi, wanatakiwa kupata uthibitisho wa ukaazi katika Nchi husika kutoka kwa Afisa wa Ubalozi wa Tanzania ili kujaza sehemu ya makazi, Mtaa/Kata kwa usahihi.
  11. Endapo Mwombaji amepata vyeti vya Shule, Namba ya mlipa kodi (TIN) na Kadi ya mpiga kura; ni vyema kuambatanisha.
  12. Mwombaji anatakiwa kujaza Fomu kwa usahihi na kuhakikisha viambata vyake na taarifa alizo jaza katika mfumo hazikinzani na taarifa nyingine, kama vile taarifa za Shule au Biashara.
  13. Mwombaji anatakiwa kujaza taarifa zake kwa usahihi, na kuchapisha taarifa hizo katika fomu na kwenda kwenye Ofisi ya Serikali ya Mtaa napoishi kwa ajili ya kugongewa Mhuri na Saini ya Mwenyekiti wa Mtaa wake.
  14. Mwombaji anatakiwa kufika katika Ofisi ya NIDA iliyoko kwenye Wilaya yake ya makazi akiwa na fomu iliyokamilika (Fomu iliyogongwa Mhuri na kuwekwa Saini ya Mwenyekiti wa Serikali wa Mtaa), pamoja na nakala ngumu za viambatisho vyake alivyopakia katika mfumo wakati wa usajili kwa ajili ya kukamilisha taratibu za usajili.
  15. Kwa Mwombaji ambaye anahitaji kupata maelezo ya ziada; asisite kufika katika ofisi ya NIDA iliyopo karibu.